Vijana wa Alliance FC leo wamewachapa wakongwe Mtibwa Sugar bao 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Nyamagana Jijini Mwanza. Bao pekee la Alliance limefungwa na Dickson Ambundo dakika ya 54 akimalizia pasi ya Michael Chinedu baada ya kipa wa Mtibwa Shaaban Kado kuutema mpira uliopigwa na Siraji Juma. Katika mchezo huo, Alliance imetawala zaidi mchezo pamoja na kufanya mashabulizi zaidi kuliko Mtibwa huku ikionekana kujiimarisha zaidi katika safu yake ya ulinzi na kudhibiti mashambulizi ya Mtibwa yaliyoongozwa na Juma Luizio, Kelvin Sabato, Ismail Mhesa na Salum Kihimbwa. Matokeo hayo yanaifanya Alliance kufikisha pointi 13 na kukaa nafasi ya 16 wakati Mtibwa ikiendelea kukaa nafasi ya nne ikiwa na pointi 23.