Goli la dakika ya mwisho ya mchezo limeiokoa Mtibwa Sugar kwa kuipa sare ya bao 1-1 dhidi ya African Lyon katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliopigwa kwenye Uwanja wa manungu Complex, mkoani Morogoro. Bao hilo la kusawazisha limefungwa na Jaffary Salum Kibaya akimalizia kwa kichwa kona iliyochongwa na Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ baada ya wageni katika mchezo huo African Lyon kutangulia kupata bao dakika ya 62 kupitia kwa mkongwe Ramadhan Chombo Redondo. Matokeo hayo yameipandisha Mtibwa kutoka nafasi ya 13 hadi nafasi ya 10 ikifikisha pointi 30 katika michezo 21 huku African Lyon ikiendelea kusalia mkiani na licha ya kufikisha pointi 20 baada ya kucheza michezo 25.